Tuesday, May 14, 2013

MGOMO WAIBUKA MIGODINI AFRIKA KUSINI BAADA YA AFISA WAO KUPIGWA RISASI.

Kampuni ya uchimbaji madini ya Lonmin, nchini Afrika Kusini inasema kuwa maelfu ya wafanyakazi katika mgodi wake wa wa platinum wamefanya mgomo kinyume cha sheria baada ya afisa wa muungano wao kupigwa risasi katika baa moja mwishioni mwa juma.
Msemaji wa kampuni hiyo Sue Vey amesema kuwa shughuli zote za uzalishaji kwenye kiwanda hicho zimevurugika .
Mgomo huu umezua hofu ya vurugu zaidi kutokea baada ya sekta hiyo kukumbwa na migomo mwaka jana
Mwezi Agosti mwaka jana wafanyakazi thelathini na wanne waliuliwa na polisi katika mgodi wa Marikana na waandishi wa habari wanasema mgomo huo umesababisha hofu ya kutokea kwa ghasia kufuatia hali ya taharuki iliyopo juu ya kukatwa kwa kazi , mashauriano ya riba na uhasama ndani ya muungano wa wafanyakazi.
Lonmin, ambayo hisa zake,ziko katika soko la hisa la London na Johannesburg , ndiyo kampuni ya tatu kwa ukubwa katika kuzalisha madini ya platinum.
Taarifa za mgomo wa leo zimesababisha hisa za kampuni hiyo kushuka kwa asilimia 5% mjini London.
Msemaji wa kampuni hiyo, Sue Vey alisema kuwa migodi yote kumi na mitatu ya kampuni hiyo imefungwa kwa sasa.
"Wafanyakazi wa kampuni hiyo waliwasili kazini ingawa hawakuelekea katika shughuli zao kama ilivyo desturi yao
Huku akisema kuwa kampuni hiyo haielewi kwa nini wafanyakazi wameamua kugoma, msemaji wa chama cha wafanyakazi hao, alisema kuwa huenda mgomo huo unatokana na ghadhabu ya wafanyakazi hao, kuhusu mauaji yaliyotokea mwishoni mwa wiki ya kiongozi mmoja wa chama hasimu cha wafanyakazi.
Polisi walithibitisha kuwa kiongozi huyo aliuawa mwishini mwa wiki katika eneo Rustenburg.

Chanzo:BBC

No comments:

Post a Comment

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...