Thursday, May 2, 2013

WASOMALIA 260,000 WAFA KWA BAA LA NJAA


Takribani raia wa Somalia 260,000, nusu yao ikiwa ni watoto, wamekufa kutokana na baa la njaa kuanzia mwaka wa 2010 hadi 2012. Hiyo ikiwa ni zaidi ya idadi ya awali kuhusu watu waliohofiwa kufa kwa wakati huo. Ripoti ya Umoja wa Mataifa imesema kuwa takribani watoto 133,000 waliokuwa na umri wa chini ya miaka mitano walikufa, huku maafisa wa Umoja  wa Mataifa wakikiri kuwa wangeweza kufanya mengi zaidi ili kujiandaa kwa baa hilo la njaa.

Ripoti hiyo ya pamoja kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo Ulimwenguni - FAO na Kitengo kinachofadhiliwa na Marekani kuhusu Baa la Njaa na Mifumo ya Tadhadhari za Mapema, ndiyo ya kwanza kabisa kutoa takwimu za utafiti wa kisayansi kuonesha idadi ya waliokufa kutokana na hali ukame wa kipindi kirefu na baa la njaa nchini Somalia.

Baa la Njaa lililiripotiwa mara ya kwanza Julai 2011 katika majimbo ya kusini mwa Somalia ya Bakool na Shabelle ya Chini, lakini baadaye likasambaa katika maeneo mengine, ikiwa ni pamoja na Shabelle ya Kati, Afgoye na ndani ya kambi za watu waliowachwa bila makaazi kutokana na vita vilivyoukumba mji mkuu Mogadishu.

SOURCE: DW.

No comments:

Post a Comment

LinkWithin

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...